1972 - 2018
Mwaka 2008, niliteuliwa kuwa Waziri wa Maji na Umwagiliaji. Awali ya hapo nilikuwa Waziri wa Nchi (Ofisi ya Makamu wa Rais) Mazingira, na kabla ya hapo, Waziri wa Mawasiliano na Uchukuzi. Moja ya changamoto kubwa ya Waziri awaye yote ni kumpata Katibu wa Waziri ambaye ndiye msaidizi mkuu, mratibu na msimamizi mkuu wa ofisi ya Waziri. Katibu Mkuu wa Wizara ambaye ndiye afisa mtendaji mkuu wa Wizara, akisaidiwa na Mkurugenzi wa Utumishi ndio wanaomsaidia Waziri katika kumpata mmoja wa watumishi waandamizi, kuwa Katibu wa Waziri. Kwa kuwa Katibu wa Waziri anafanya kazi na Waziri, basi anayependekezwa lazima akubalike na Waziri.
Katibu ndiye anayepanga ratiba ya kazi ya Waziri. Katibu wa Waziri ndiye anayewaona kwanza wageni wote wa Waziri. Katibu ndiye anayechukua kumbukumbu ya vikao vyote vya Waziri. Katibu wa Waziri ndiye kiungo cha muda wote kati ya Waziri na watendaji wa Wizara. Ingawa Katibu Mkuu na Naibu Waziri au Mawaziri wenzake wana mawasiliano ya moja kwa moja, Katibu wa Waziri ndiye atakayefuatilia utekelezaji wa yale yatokanayo. Kwa kuwa ofisi ya Waziri huwa na mawasiliano ambayo kwa mujibu wa taratibu ni SIRI, ikiwa ni pamoja na nyaraka za Baraza la Mawaziri, Katibu wa Waziri lazima afanyiwe upekuzi na vyombo vinavyohusika.
Ni dhahiri kutokana na yaliyotangulia kwamba Katibu wa Waziri ni mtu muhimu sana katika Wizara. Lazima awe mchapakazi, ikiwa ni pamoja na kuchapakazi nje ya saa za kazi. Lazima awe mwadilifu, mwaminifu, na awe tayari kumshauri Waziri ipasavyo bila kujali Waziri ataupokeaje ushauri huo, ili mradi ni wa manufaa kwa Wizara na Taifa.
Hivi ndivyo nilivyo kubali ushauri wa aliyekuwa Katibu Mkuu wa Maji na Umwagiliaji alivyopendekeza, nami nikakubali, uteuzi wa Ngusa Izengo, kuwa Katibu wangu. Sifa zote zilizo hapo juu zilimlenga yeye. Zaidi ya hayo Ngusa alikuwa mnyenyekevu, hana makuu, rafiki wa kila mtu, awe mdogo au mkubwa, kwa umri au kwa cheo. Chuki na hasira havikuwemo kabisa katika istilahi ya lugha yake. Aliizoea, bila kinyongo au kulalamika, ratiba yangu ya kazi iliyokuwa ngumu, watumishi wanapoondoka kurudi makwao saa 9.30 mchana, ndio kwanza tunaaza kazi mpaka saa 3 usiku kama tukiwahi. Safari za ghafla ni za kawaida kwa Waziri. Vikao vya dharura vinaweza kuitishwa ama Ikulu, Dar es Salaam, au Dodoma, na Katibu alikuwa tayari wakati wowote.
Tanzania labda ni nchi pekee katika kanda yetu ambapo hata Mkuu wa Nchi anajua, kuhusiana na ujenzi kwamba Zege Halilali. Msemo huu wa wajenzi niliutafsiri kwamba kazi inayobidi kumalizika leo, iishe leo. Niliwakumbusha watendaji kuwa Baba wa Taifa, Mwalimu Nyerere, alituasa kwamba Linalowezekana kufanywa leo, lisingoje kesho. Ngusa aliusimamia vilivyo mwongozo huu, ndani ya ofisi na kwa wale waliohusika na utekelezaji wa maelekezo ya Waziri. Ilimgharimu muda na afya. Lakini alitekeleza wajibu wake ipasavyo.
Kama ilivyokuwa kwa watendaji wote tuliofanya kazi pamoja, pamoja na ufinyu wa muda, nilimshauri asiishie na shahada ya uhandisi tu bali ajiendeleze zaidi. Ushauri huu aliuzingatia na akajiandikisha Chuo Kikuu cha Dar es Salaam na kuhitimu shahada ya uzamili katika usimamizi wa uhandisi.
Taratibu za Serikali zinamtaka Waziri anapohama asihame na wasaidizi wake. Hata hivyo ilibidi nijenge hoja kwa Katibu Mkuu mwenye dhamana ya Utumishi aruhusu Ngusa aende na mimi Ikulu. Kwani mwaka 2012 niliteuliwa kuwa Waziri wa Nchi (Ofisi ya Rais) Kazi Maalum.
Ukaribu wa Waziri na Katibu wake unamfanya Katibu awe karibu sana na familia ya Waziri. Hakika Ngusa alikuwa sehemu ya familia ya Mwandosya. Kwa maana hii kifo cha Ngusa kimetusikitisha wote katika familia: Mimi na Mama, na vijana wetu, Max, Sekela na Emmanuel; Godfrey na Joyceline na familia yao; Wananchi wa Busokelo (Rungwe Mashariki); Wizara ya Maji na Umwagiliaji; Ikulu; Halmashauri na wananchi wa Wilaya ya Kongwa; na Watendaji wengi ndani na nje ya nchi. Kama alivyokuwa mwanafamilia, sisi tutashauriana na familia ya Marehemu Ngusa Izengo kuona ni jinsi gani tunaweza kuwajibika katika kuhakikisha watoto wa Ngusa wanaendelea kupata elimu bora.

Walioketi: kushoto Prof. Mark Mwandosya, kulia Mama Christina Nsekela.
Nikiwa katika matibabu huko Hyderabad, India, Ngusa alikuja kunijulia hali. Alinikuta katika hali mbaya, nikiwa siwezi kutembea. Nakumbuka Ngusa akisema “Mheshimiwa, mimi naamini utapona kabisa na utaanza kutembea tena. Maadui zako na hao waliokuzushia kifo watashangaa kabisa”.

Ngusa Izengo, kulia, akichukua picha ya pamoja na Prof. Mark Mwandosya, kushoto, na Mama Lucy Mwandosya, alipoenda kumjulia hali Waziri Mwandosya, alipokuwa matibabu, Hospitali ya Apollo, Hyderabad, India. Hii ilikuwa mwaka 2011.
Kwa mujibu wa Maelezo Binafsi ya Marehemu, Ngusa Laurent Izengo alizaliwa tarehe 14 Aprili 1972 huko Chato, Geita. Alianza elimu Shule ya Msingi Mweri mwaka 1981 na kuhitimu darasa la saba mwaka 1987. Elimu ya sekondari aliipata Shule ya Sekondari ya Lake, Mwanza, kidato cha kwanza mpaka kidato channe, 1988-1992, na Shule ya Sekondari Kibaha, 1993-1995. Baada ya hapo alijiunga na Chuo Kikuu cha Dar es Salaam mwaka 1996 na kufuzu shahada ya kwanza ya Uhandisi Ujenzi mwaka 2000. Marehemu ameacha mke, Flora Lyambogo Izengo, na watoto wawili, Augustine Izengo, na Hellen Izengo.
Waliosimama, kuanzia kushoto: Ngusa Laurent Izengo, Mama Lucy Mwandosya, Baba Askofu Israel-Peter Mwakyolile, Mama Mchungaji Mwakyolile, Baba Askofu Lusekelo Mwakafwila, na Mama Mwakafwila, tulipomtembelea Mama Nsekela, kijijini Kalalo Juu, Kyimo, Rungwe.Picha ilipigwa 2015.
Nikiwa katika matibabu huko Hyderabad, India, Ngusa alikuja kunijulia hali. Alinikuta katika hali mbaya, nikiwa siwezi kutembea. Nakumbuka Ngusa akisema “Mheshimiwa, mimi naamini utapona kabisa na utaanza kutembea tena. Maadui zako na hao waliokuzushia kifo watashangaa kabisa”.

Ngusa Izengo, kulia, akichukua picha ya pamoja na Prof. Mark Mwandosya, kushoto, na Mama Lucy Mwandosya, alipoenda kumjulia hali Waziri Mwandosya, alipokuwa matibabu, Hospitali ya Apollo, Hyderabad, India. Hii ilikuwa mwaka 2011.
Kwa mujibu wa Maelezo Binafsi ya Marehemu, Ngusa Laurent Izengo alizaliwa tarehe 14 Aprili 1972 huko Chato, Geita. Alianza elimu Shule ya Msingi Mweri mwaka 1981 na kuhitimu darasa la saba mwaka 1987. Elimu ya sekondari aliipata Shule ya Sekondari ya Lake, Mwanza, kidato cha kwanza mpaka kidato channe, 1988-1992, na Shule ya Sekondari Kibaha, 1993-1995. Baada ya hapo alijiunga na Chuo Kikuu cha Dar es Salaam mwaka 1996 na kufuzu shahada ya kwanza ya Uhandisi Ujenzi mwaka 2000. Marehemu ameacha mke, Flora Lyambogo Izengo, na watoto wawili, Augustine Izengo, na Hellen Izengo.
Kwa familia ya Ngusa, wazazi, mke na watoto, ndugu na marafiki, maneno ya faraja hatunayo. Kwani kwa lolote tutakalosema halitamrudisha Ngusa. Faraja tuliyonayo, na Kama Mfalme Daudi alivyonena katika Agano la Kale, na bila kuharibu maana ya maneno yake: Ngusa ametutoka. Huko aliko hawezi kurudi. Bali faraja tuliyonayo ni kwamba sisi tutaenda huko aliko. Itakuwa furaha iliyoje tutakapoonana naye katika mtaa wa amani ya milele huko mbinguni. Basi wafiwa, ndugu zangu, Mwenyezi Mungu atupe subira, na tuendelee kufarijiana.
Mwenyezi Mungu Amrehemu Ngusa Izengo.
Bwana Alitoa, Bwana Ametwaa. Jina la Bwana lihimidiwe.
Inna Lillahi wa Inna Ilaihi Rajiun.
Mark Mwandosya
Lufilyo
Busokelo
16 Aprili 2018
![]() |
Ngusa Izengo, kulia kwa mama, akiwa na Profesa Mark Mwandosya na Mama Lucy Mwandosya wakiwa mpakani mwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo na Rwanda (Goma na Gisenyi). |
Rest in eternal peace Ndugu Izengo.
ReplyDelete