Skip to main content

UJUMBE WA TASIHILI (A VALEDICTORY MESSAGE) KWA CHUO KIKUU CHA SAYANSI NA TEKNOLOJIA MBEYA (MUST)


UJUMBE WA TASIHILI (A VALEDICTORY MESSAGE) KWA CHUO KIKUU CHA     SAYANSI NA TEKNOLOJIA MBEYA (MUST)



Naanza kwa kuishukuru Mamlaka ya Uteuzi kwa kuniwezesha kuwa Mkuu wa Chuo Kikuu cha Sayansi na Teknolojia Mbeya kuanzia 2014 mpaka 2018. Aidha nawapongeza, Mhe. Pius Msekwa na Mhe. Zakia Meghji, kwa uteuzi wao kuwa Mkuu wa Chuo, na Mwenyekiti wa Baraza la Chuo, mtawalia. Nawatakia kila la heri katika ulezi na usimamizi wa Chuo.

Pili, ingawa nauita ushauri, kwa kweli ni ujumbe wa shukrani kwa Mamlaka ya Uteuzi na maelezo mafupi kuhusu uzoefu mdogo nilioupata nikiwa Mkuu wa Chuo Mwanzilishi wa Chuo Kikuu cha Sayansi na Teknolojia Mbeya (MUST). Kwani nitawezaje kutoa ushauri kwa Mkuu wa Chuo ambaye muda wake mrefu wa utumishi wake kwa Umma amekuwa katika maendeleo ya elimu ya juu, akiwa Makamu Mkuu Mwanzilishi wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, na Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Kwa maana hiyo MUST itafaidika pia kutokana na uzoefu na utumishi wa muda mrefu katika ngazi za juu wa Mkuu wa Chuo, na Mwenyekiti wa Baraza, ambaye naye amewahi kuwa Mwenyekiti wa Mashirika mbalimbali, Mbunge, Mkuu wa Mkoa na Waziri. 

Niliteuliwa na Mheshimiwa Rais mwezi Aprili 2014 kuwa Mkuu wa Chuo Kikuu cha Sayansi Teknolojia Mbeya Mwezi Aprili 2014 kwa mujibu wa Kifungu cha 35 cha Sheria ya Vyuo Vikuu, Sheria Na 7 ya Mwaka 2005, kikisomwa pamoja na “Charter” ya MUST, na kuhitimisha muhula wangu Mwezi Novemba 2018, mara tu baada ya uteuzi wa Mkuu wa Chuo mpya. Ilinichukua miaka miwili kukifahamu vizuri Chuo na kuniwezesha kutoa ushauri kuhusu utekelezaji wa dira na jinsi nilivyoona nini ungekuwa wajibu wa Chuo katika kutekeleza matarajio ya Nchi tunapoelekea mwishoni mwa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2025. Ushauri huo niliutoa Chuoni, katika Mhadhara, Ijumaa tarehe 16 Desemba 2016(Science Technology and Society: The Potential of Mbeya University of Science and Technology in Realizing the Goals of Vision 2025)  (http://www.markmwandosya.com/2017/08/chancellors-inaugural-lecture-by-prof.html). Kwa muhtasari tu, pamoja na mengine, nilishauri mambo yafuatayo:

(1)  Umuhimu wa MUST katika maendeleo ya sayansi, teknolojia na ubunifu katika muktadha wa Dira ya Maendeleo ya Taifa 2025. Kwa kiwango kikubwa nilirejea hotuba muhimu aliyoitoa Mwalimu Nyerere alipokuwa akizindua Chuo Kikuu cha Dar es Salaam mwaka 1970.

(2)  Umuhimu wa MUST katika maendeleo ya jamii inayokizunguka Chuo. Katika hili nilishauri Chuo kijipime uwezo wake kwa jinsi kunavyoweza kuhusika na maendeleo ya elimu, sayansi na teknolojia katika mazingira ya kijiji, kata, Jiji la Mbeya na Nyanda za Juu za Kusini. Aidha, naendelea kushauri MUST iboreshe miundombinu ya ndani, majengo na barabara, pamoja na barabara kutoka TAZARA kupitia kijiji cha Ikuti, kama njia ya mafunzo kwa vitendo. Haitaeleweka kwa chuo kikuu cha sayansi na teknolojia kulalamika kuhusu ubovu wa miundombinu katika eneo lake.

(3)  Kutokana na (2) hapo juu, kuwa na ushirikiano na vyuo vilivyo karibu MUST vyenye mwelekeo unaoshabihiana katika sayansi na teknolojia. Ushauri huu umewezesha MUST kuanzisha masomo ya ufundi na uhandisi katika teknolojia ya sekta ya afya (Biomedical Technology), kwa kushirikiana na Hospitali ya Kanda ya Rufaa iliyo Mbeya. Kuna uhaba mkubwa wa mafundi na wahandisi wa vifaa vya matibabu nchini. Aidha katika azma hii ya ushirikiano, MUST na Taasisi ya Kilimo cha Uyole wanaandaa rasimu ya  makubaliano. Uyole na MUST ziko katika kanda muhimu ya uzalishaji wa mazao ya kilimo nchini. Uangaliwe uwezekano wa kuanzisha mafunzo ya agricultural mechanization and agricultural engineering kwa ushirikiano na Taasisi ya Uyole. Nimezungumza na Mkurugenzi wa Uhandisi-Kilimo, Wizara ya Kilimo, amevutiwa sana na hoja ya kuishirikisha MUST na vyuo vya elimu ya juu katika kuandaa na kutekeleza sera ya matumizi ya teknolojia katika kuinua uzalishaji wa kilimo. Wizara ya Kilimo itakuwa tayari kuikabidhi MUST kituo cha teknolojia katika kilimo kilichopo Mbarari kilichoanzishwa kwa msaada wa Japan. Nashauri MUST iendeleze mazungumzo haya kwa manufaa ya Chuo na Taifa. Aidha, nazidi kushauri kuanzishwe mafunzo ya uhandisi katika fani ya reli ili kutayarisha raslimali watu kwenye sekta inayokua hasa sasa Taifa linapoekeleza mradi wa Standard Gauge Rail (SGR).Ushirikiano na TAZARA ikiwa ni pamoja na matumizi ya karakana ya TAZARA iliyo Mbeya utahitajika katika suala hili.

(4) Ushirikiano na vyuo vingine vya sayansi na teknolojia nchini. Vyuo vifuatavyo vimeanzishwa kitaifa mahususi kwa maendeleo ya sayansi na teknolojia: Taasisi ya Teknolojia Dar es Salaam (DIT); Chuo cha Ufundi Arusha (ATC); Taasisi ya Nelson Mandela ya Sayansi na Teknolojia Afrika (NM-IST), Taasisi ya Uchukuzi (NIT); na Chuo Kikuu cha Sayansi na Teknolojia Mbeya (MUST). Vyuo hivi vina nafasi kubwa ya ushirikiano katika mafunzo, ushauri, utafiti wa pamoja na kubadilishana walimu na wanafunzi kwa vipindi, hasa kutokana na uchache wa walimu wenye fani za kipekee na vifaa. Navilinganisha vyuo hivi na mfumo wa vyuo kama hivi huko India, Indian Institute of Technology, New Delhi, Madras, Hyderabad, na kwingineko ambako Serikali ya India imeweka mkazo maalum ulivyovifanya vyuo hivyo kuwa na mchango mkubwa katika maendeleo ya sayansi na teknolojia India na ulimwenguni. Nashauri uangaliwe mfumo utakaoviwezesha vyuo vyetu (Institutes of Technology Tanzania-ITTs) kuwa na uratibu wa pamoja bila kuathiri uhuru wa kila chuo, ili kuendeleza sayansi na teknolojia kwa kasi na ufanisi zaidi.

(5)  Ushirikiano na vyuo vingine nchini na duniani. Uelewa, elimu na ujuzi havina mipaka ya kijiografia wala kisiasa. Hivyo basi, ni muhimu MUST ikajenga uhusiano na vyuo vingine nchini na duniani kote. Mbali na umuhimu huo, MUST inaweza ikafaidika na misaada mingi inayotolewa kupitia programu za pamoja za mafunzo na utafiti. Ili kutekeleza azma hii niliona ni wajibu wangu, kila nilipopata nafasi ya kusafiri nje ya nchi kwa shughuli nyingine tu, kupanga na kuongea na wawakilishi wa vyuo mbalimbali kuhusu uwezekano wa ushirikiano baina yao na MUST. Baadhi ya vyuo hivyo ni: Chuo Kikuu cha Virginia, Marekani; Chuo Kikuu cha Hartford, Marekani; Chuo Kikuu cha Sayansi na Teknolojia cha Adama, Ethiopia; Chuo Kikuu cha Mountains of the Moon, Uganda; Institute of Science and Technology Hyderabad, India; University ofRwanda; Rwanda Polytechnic Institute; University of Comoro; National University of Science and Technology, Zimbabwe; Bindura University, Zimbabwe; na vyuo nilikohitimu, University of Aston na University of Birmingham, Uingereza. Kufikia Desemba 2018 MUST ilikuwa katika hatua mbalimbali za mawasiliano ya kuanzisha ushirikiano.

(6)  Ushirikiano na Taasisi, Kampuni na Mashirika nchini. Chuo kikuu cha uhandisi na sayansi kinahitaji kuwa na uhusiano na ushirikiano na taasisi, kampuni na mashirika ambayo yanaweza kuajiri wahandisi wanaohitimu chuoni na wanaweza kupokea wanafunzi wa mafunzo ya mazoezi ya muda mfupi. Hivyo basi nilona ni wajibu wangu kuwaunganisha MUST na baadhi ya taasisi nilizofanya nazo kazi katika utumishi wa umma. Baadhi ya hizo ni: Mamlaka ya Udhibiti wa Mawasiliano Tanzania (TCRA); Mfuko wa Mawasiliano kwa Wote, Wakala wa Umeme Vijijini; Kampuni ya Simu TIGO; Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC); na Shirika la Maendeleo la Korea ya Kusini.

(7) Mfuko wa Maendeleo ya Sayansi, Teknolojia, Uhandisi, Hisabati na Ubunifu kwa Wanawake. Takwimu zinadhihirisha uchache mkubwa wa wasichana/wanawake wanaopata udahili katika fani za sayansi na uhandisi nchini na sehemu nyingi duniani. Ili kupunguza tofauti hiyo, ushauri ulitolewa na Baraza likaanzisha Mfuko maalum ili MUST iweze ikasaidia wasichana wanaokidhi na kuzidi vigezo lakini hawana uwezo wa kifedha. Baadhi ya taasisi zilizo katika (6) hapo juu zimechangia katika kuanzisha Mfuko huo wa Mkuu wa Chuo. Pamoja na Mfuko, Chuo kimeanzisha utaratibu wa kutembelea shule za sekondari mkoani Mbeya ili kuwaelimisha wanafunzi, hasa wa kike kuhusu umuhimu wa masomo ya sayansi na hisabati katika maendeleo ya nchi. Naamini Mkuu wa Chuo na Mwenyekiti watauinua mfuko huu kwa kuwahusisha washirika wao wengi wa maendeleo.

(8) Mfululizo wa Mihadhara ya Mkuu wa Chuo. Ili kukiunganisha Chuo na Wasomi na wataalam wa aina na fani mbalimbali, na kama ilivyo jadi na uzoefu wa vyuo vikuu, ushauri ulitolewa na Baraza likapitisha uamuzi wa kuwa na mihadhara hiyo. Nashauri Baraza lipitishe sera na utaratibu wa zoezi hili muhimu ili lisihusishwe na Mkuu wa Chuo aliyepo, na liwe la kudumu. Kwa bahati mbaya Msomi wa kutoa Mhadhara wa mwaka 2018 na waalikwa walipewa notisi ya saa 12 ya kuahirishwa kwa Mhadhara ambao tayari ulikuwa umetangazwa.

(9) Shahada ya Heshima (Honoris Causa).Ni jadi na kawaida ya vyuo vikuu duniani kote kuwatambua watu walioweza kuchangia maendeleo ya elimu, uelewa, utafiti na maendeleo ya jamii. Nilishuri na Baraza likaafiki kuanzisha sera na utaratibu wa Chuo kutoa Shahada ya Heshima. Kamati husika ilikaa na kutoa mapendekezo kwa Seneti ambayo pia ilitoa mapendekezo kwa Baraza ambalo kwa mujibu wa taratibu lilipendekeza majina matau kwa Mkuu wa Chuo: Mhandisi Joseph Simbakalia; Mhandiisi Profesa Awadhi Sadiki Mawenya; na Mhandisi Profesa Matthew Luhanga. Kutokana na mchango wake mkubwa katika elimu ya uhandisi, ikiwa ni pamoja na kuwa mwanzilishi na Mtanzania wa kwanza kuwa Profesa na Mkuu wa Kitivo cha Uhandisi Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, na Mtanzania wa kwanza kupata Udaktari wa Falsafa katika Uhandisi, Mwanzilishi wa Institution of Engineers Tanzania, Mwanzilishi wa Engineers Registration Board,Mwanzilishi wa Tanzania Academy of Sciences, na Mwanzilishi wa Front Against Corruption in Engineering in Tanzania, Mkuu wa Chuo alimteua Mhandisi Profesa Awadhi Sadiki Mawenya kutunukiwa shahada hiyo. Mhandisi Mawenya alitaarifiwa rasmi na kualikwa kwenye Mahafali. 

(10)  Bustani ya Mimea. Mtakuwa mmetaarifiwa kwamba MUST ina eneo kubwa na lakutosha kwa miaka mingi ijayo, hata karne. Ni hekta 1001 au ekari 2500 kampasi ya Iyunga na hekta 48 kampasi ya Kianda, Rukwa. Kwa upande wa Kampasi ya Iyunga, eneo lote limepata hati miliki. Hata hivyo, eneo lenye hekta 511 bado wananchi hawajafidiwa. Serikali iombwe kuwafidia wananchi mapema iwezekanavyo ili eneo lote lichukuliwe na Chuo kwa maendeleo yake. Chuo kina mpango wa kuongeza eneo la Kampasi ya Kianda kufikia hekta 500. Kwa muda mrefu neo kubwa litabaki bila matumizi. Chuo Kikuu cha Dar es Salaam kiliacha maeneo kama hayo yawe msitu na mengine kutumika kwa njia mbali mbali kwa ajili elimu ya mimea na wanyama, na ikawa vigumu eneo lao kuingiliwa. Kwa MUST eneo kubwa ni mashamba ya wafanyakazi na wananchi. Nimeshauri na limetengwa eneo dogo kwa ajili ya bustani ya mimea (Botanical Garden). Bustani itasaidia kuboresha mandhari ya Chuo, kuwa mahali ambapo wanafunzi watapumzuka na kujisomea, na jamii ya chuo kujifunza sayansi ya mimea. MUST ikifanikisha azma hii, Bustani tarajiwa itakuwa ni ya kipekee nchini. Aidha, kwa kuwa itachukua miaka mingi kutekeleza mpango wa Chuo wa maendeleo wa ardhi, nashauri ipandwe miti kwenye mipaka na  ndani ya eneo kubwa la Chuo ili kuzuia uvamizi wa maeneo ya wazi ya ardhi hiyo. Kwani “Asilia haivumilii ombwe”.

Namalizia na mambo matatu ambayo yanashabihiana na yaliyotangulia. Mosi, taratibu za kuhuisha uongozi wa Chuo ziko katika Kifungu 36 na Kifungu 37 Sheria ya Vyuo Vikuu, kwa ajili ya uteuzi wa Makamu Mkuu wa Chuo, na Naibu Makamu wa Mkuu wa Chuo, sawia, na “Charter” ya MUST. Baada ya kuangalia mahitaji ya uongozi katika ngazi za Makamu Mkuu wa Chuo na Naibu Makamu wa Chuo, mwishoni mwaka 2017 Baraza liliunda Kamati ya Uteuzi (Nominations Committee) ambayo Mwenyekiti wake aliteuliwa na Mkuu wa Chuo. Baada ya Kumaliza kazi Kamati ikapeleka Ripoti yake kwenye Baraza. Baada ya hapo mapendekezo yalipelekwa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia mwezi Januari 2018. Taratibu zinahitaji majina yanayopendekezwa yapelekewe Ikulu kwa upekuzi na hatua nyingine. Mwezi Novemba 2018 Wizara ilileta mapendekezo ya mwisho kwa ajili ya uteuzi. Mapendekezo hayo yalirudi tena kwenye Baraza, ambalo nalo likayapitisha na kumpelekea Mkuu wa Chuo kwa uteuzi rasmi. Uteuzi umefanyika kama ilivyo pendekezwa. Prof. Aloys Mvuma kutoka Chuo Kikuu cha Dodoma, ameteuliwa kuwa Makamu Mkuu wa Chuo; Prof. Justinian Anatory, kutoka Chuo Kikuu cha Dodoma, ameteuliwa kuwa Naibu Makamu Mkuu wa Chuo (Fedha, Mipango na Ushauri) na Prof. Godliving Mtui, kutoka Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, ameteuliwa kuwa Naibu Makamu Mkuu wa Chuo (Taaluma na Utafiti). Naamini mnaanza na uongozi thabiti wa kukabiliana na changamoto katika kipindi muhimu cha kutoka Chuo na Taasisi ya Ufundi kuwa Chuo Kikuu cha Sayansi na Teknolojia, na jinsi teknolojia inavyokua kwa kasi.

Pili, Chuo hakina Maktaba yenye hadhi ya Chuo Kikuu. Jengo linaendelea kujengwa. Mkuu wa Chuo amewaunganisha uongozi wa Chuo na ule wa Wakala wa Majengo ya Serikali. Naamini ujenzi utakamilika mapema. Hata hivyo, Mheshimiwa Waziri wa Elimu amevitahadharisha vyuo kuhusu ufinyu wa bajeti ya serikali na kuvitaka vijitahidi kutumia vizuri vyanzo vyao vya ndani kwa shughuli za maendeleo. Nashauri mtazamo huu utumike katika kukamilisha Maktaba ya MUST. Katika suala la matumizi ya Maktaba inashauriwa MUST izingatie mabadiliko yanayotokana na maendeleo makubwa ya teknolojia ya habari. Kwa kuanzia familia yangu imewakabidhi MUST vitabu 1032 vya taaluma vya kielektroniki. Tutaendelea kuchangia maendeleo ya Chuo kwa kadri itakavyowezekana.

Tatu, na mwisho, ni changamoto ambazo nawapa, kama ushauri tu, MUST na ITTsnyingine:
(1)   Katika muktadha wa kufikia maendeleo ya kati kama ilivyo kwenye Dira ya Taifa ya Maendeleo 2025, tumedhamiria kuwa Taifa la Viwanda. Dunia ya sasa iko katika Mapinduzi ya Nne ya Kiviwanda (the Fourth Industrial Revolution). Wajibu wa MUST na ITTs ni kuishauri Serikali na kutayarisha rasilimali watu na jamii iliyojikita katika uelewa wa teknolojia (cutting edge technology) inayoendana na mapinduzi haya. Teknolojia hizi ni pamoja na Nanotechnology, biotechnology, artificial intelligence, information technology including 5th generation wireless and Internet of Things, blockchain technology and 3D Printing (kwa pamoja ni cyber-physical systems, an interaction of digital, physical and biological systems).Vinginevyo dunia itaenda mbele wakati sisi tukijikita katika Mapinduzi ya II ya Kiviwanda (the Second Industrial Revolution) na Mapinduzi ya III ya Kiviwanda (the Third Industrial Revolution). 
(2)  Changamoto ya pili ni mahususi zaidi. Mwaka 2021 Tanzania itasherehekea miaka 60 ya Uhuru wa Tanganyika. Ni wakati mzuri wa kuwa na jambo letu ambalo wanasayansi na wahandisi wetu wanaweza kuutangazia umma na ulimwengu jambo ambalo tumefanikisha. Pamoja na mengine, nashauri tuangalie uwezekano wa kutengeneza “satellite” ya mawasiliano au hali ya hewa na kuirusha kupitia roketi za India mwaka 2021.  Nimezungumza na Waziri wa Ujenzi, Mawasiliano na Uchukuzi na amekubali kwamba hatua hii   ingekuwa ya maana na yenye heshima kwa Nchi. MUST kwa ushirikiano na ITTs nyingine nchini, Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Wizara ya Elimu na Wizara ya Ujenzi, Mawasiliano na Uchukuzi, wanaweza kuangalia uwezekano wa kutekeleza azma hii. Kwa wengi wenu wazo hili linaweza likaonekana kama jambo la ajabu. Hebu fikirieni, siku hizi huko India na sehemu nyingine duniani "satellite" zinatengenezwa na wanafunzi wa sekondari na kurushwa angani kutumia roketi za India na nchi nyingine
 (https://www.timesofindia/india/75-students-satellites-in-space-by-2022... na https://www.bbc.com/news/ world/asia-india-46956595?ocd=wsnews...).
    Katika azma hii majirani zetu Rwanda wametutangulia.    Kwani wanatarajia, kwa kushirikiana na mashirika ya    nje, kurusha "satellite" angani mwaka 2019 (https://face2faceafrica.com/article/rwanda-set-to-launch-africas-latest-space-satellite-in-2019).


Nawasihi wanafunzi: waongeze bidii na juhudi katika masomo; wawe na udadisi katika kutafuta uelewa na ukweli; wawe wabunifu na wachambuzi wa kina katika changamoto zinazowakabili wao na jamii; wawe na ujasiri wa kusimamia haki na katika yale wanayoamini; wawe na uhodari wa kujenga hoja na kutoa sababu za msingi katika kufanya hivyo, ikiwa ni pamoja na kujikita katika marejeo muhimu; na waoneshe uzalendo katika fikra na matendo ili kujiandaa kulitumikia Taifa. Kwa kufanya hivyo umma unaweza kuwatambua na kuwatukuza kwa kusema “hili hakika ni zao la MUST”. 

Naishukuru jumuiya ya MUST: Prof. Penina Mlama, aliyekuwa Mwenyekiti wa Baraza la Chuo; Dr. Amos Nungu ambaye alikuwa Kaimu Mwenyekiti wa Baraza la Chuo; Wajumbe wote wa Baraza la Chuo; Uongozi; Wahadhiri; Wakufunzi; Wafanyakazi na Wanafunzi; kwa ushirikiano walionipa kwa kipindi chote nilichopata heshima ya kuwa Mkuu wa Chuo.

Nahitimisha kama nilivyoanza, kwa kumshukuru Mheshimiwa Rais kwa kuniwezesha kuwa Mkuu wa Chuo kuanzia 2014 mpaka 2018, na kumpongeza Mhe. Pius Msekwa, Mkuu wa Chuo, na Mhe. Zakia Meghji, Mwenyekiti wa Baraza la Chuo kwa uteuzi wao, na kuwatakia kila la heri katika ulezi na usimamizi wa Chuo.





Mark J. Mwandosya
Lufilyo
Busokelo
Wilaya ya Rungwe
2 Januari 2019

 
Prof Mwandosya na Prof Mlama.














Copyright© 2017 Mark Mwandosya. All rights reserved

Comments

  1. Hakika Ushauri wako ni mzuri saana si tu kwa MUST bali na kwa vyuo vingine si tu kwa wanafunzi wa MUST bali ni kwa wanafunzi wa TANZANIA na Nchi nyingine zinazoendelea.

    ReplyDelete
  2. Hakika Ushauri wako ni mzuri saana si tu kwa MUST bali na kwa vyuo vingine si tu kwa wanafunzi wa MUST bali ni kwa wanafunzi wa TANZANIA na Nchi nyingine zinazoendelea.

    ReplyDelete
  3. Sijui nikupongezeeee!! Lakini wacha NIKUSHUKURU mosi, kwa kutushirikisha mawazo haya mazuri sana ambayo nadhani yana tija si kwa MUST na TTT (Taasisi za Teknolojia Tanzania) bali sisi sote popte tulipo kwa nafasi mbali mbali. Lakini zaidi kwa Kuonesha njia juu ya kuishirikisha jamii pana kuhusu mawazo ambayo iwapo ungeyatoa kwenye ukumbi wa chuo pekee, pasi tusingenufaika.

    ReplyDelete
  4. Babu mchango wako katika Taifa la Tanzania ni nuru na ni chachu ya maendeleo, Mungu akubariki na hakupe maisha marefu.

    ReplyDelete
  5. Great speech...many thanks prof.

    ReplyDelete
  6. Great speech...many thanks prof.

    ReplyDelete
  7. Prof. pongezi nyingi sana kwa waraka uliosheheni maono makubwa yenye uhalisia na ya kisasa kabisa unapoyapima kwenye nyanja za kiteknolojia pia. MUST wakiyazingatia yatawainua na kuwaweka juu kabisa kwenye orodha ndefu ya vyuo vikuu kama'center of excellence'' Pongezi nyingi tena kwa uzalendo.
    Owden Andalwisye Mwaikema.

    ReplyDelete

Post a Comment

Popular posts from this blog

Salaam kutoka Comoro

Nimeona niandike waraka huu kutoka ughaibuni, ingawa si ugenini sana, nikiwa Jamhuri ya Comoro. Nimebahatika kusafiri sana kikazi duniani kote, kuanzia Japan mpaka Brazil, kuanzia Guyana mpaka Australia. Nimeiwakilisha nchi kikazi katika mabara yote isipokuwa Aktiki na Antaktika. Namshukuru Rabuka kwa kuniwezesha kulitumikia Taifa langu kwa zaidi ya miaka arobaini. Nimetembelea nchi zote jirani isipokuwa Jamhuri ya Comoro. Mara nyingi tumezoea kusema Tanzania inapakana na nchi nane; Kenya, Uganda, Rwanda, Burundi, Jamhuri ya Watu ya Congo, Zambia, Malawi, na Msumbiji. Tunasahau kwamba watu wa Visiwa vya Comoro ni jirani zetu. Badala ya mpaka wa ardhi tunatenganishwa na Bahari ya Hindi. Inawezekana hii ikawa ndio sababu ya nchi zetu kutokuwa na ushirikiano wa karibu kiuchumi na kiutawala, pamoja na kwamba kijamii na kiutamaduni sisi, na hasa watu wa mwambao wa pwani na Zanzibar, Wacomoro wamekuwa ni sehemu yetu. Mara nyingi utasikia fulani na fulani wametutangulia mbele

Grüße aus Matema Beach, Nyasa See, Tansania

Grüße aus Matema Beach, Nyasa See, Tansania Von Mark Mwandosya. 26. Oktober 2017 (Übersetzt von Heinke Schimanowski-Thomsen) Vorwort Im August 2017 hatte ich Gelegenheit zur Republik der Komoren Inseln zu reisen. Die Komoren bestehen aus 4 Inseln: Grande Comore (Ngazija), Anjouan (Nzuwani), Mohéli (Mwali) und Mayotte (Mahoré). Die Insel Mayotte steht weiterhin unter französischer Verwaltung solange bis  die Einwohner entscheiden, sich mit den anderen Inseln zu vereinigen. Die Komoren beanspruchen die Insel Mayotte als zu ihrer Einheit zugehörig. Ich und meine Familie besuchten 2 Inseln von diesen 4, Ngazija und Nzuwani. Als ich auf den Komoren war verfasste ich einen Brief, den ich „Grüße von den Komoren“ nannte und im Netz veröffentlichte. Viele Leute hatten Gelegenheit diesen Brief zu lesen. Einige von denen, zusammen mit Glückwünschen, rieten mir, so einen Brief über Tansania zu schreiben. Das war für mich eine Herausforderung. So einen Brief zu schrei

Salaam kutoka Matema Beach, Ziwa Nyasa, Tanzania

Salaam kutoka Matema Beach, Ziwa Nyasa, Tanzania Utangulizi Mwezi Agosti 2017 nilipata nafasi ya kusafiri kwenda Jamhuri ya Visiwa vya Comoro. Comoro ni umoja wa visiwa vinne; Ngazija, Nzuwani, Mwali, na Maore. Hata hivyo kisiwa cha Maore au Mayotte kinasimamiwa na Ufaransa mpaka hapo wananchi wa Maore watakapoamua kuungana na visiwa vingine. Comoro inaendelea kukitambua kisiwa cha Maore kama sehemu ya Umoja wake. Mimi na familia yangu tulizuru visiwa viwili kati ya hivyo vinne, Ngazija na Nzuwani. Nikiwa Comoro niliandika waraka niliouita “Salaam kutoka Comoro” na kuusambaza katika mtandao. Watu wengi wamepata nafasi ya kusoma waraka huo. Baadhi yao, pamoja na kunipongeza walinishauri, na hakika walinipa changamoto kuhusu umuhimu wa kuandika waraka kama huo lakini ukilenga kuitangaza Tanzania, kwa watanzania na wageni. Unaanzia wapi kuandika kuhusu Tanzania, nchi iliyojaaliwa na Mwenyezi Mungu kuwa na rasilimali asilia zisizo na mfano duniani? Aidha watu wengi wameandika